Unachofanya unakielewa au unafanya ilimradi uonekane umefanya?

Habari za leo mpenzi msomaji wa MTAZAMO WA MAISHA, ni matumaini yangu umeanza siku na mwezi huu vyema wa tisa ukiwa na mipango mingi ya kusogea hapo ulipo na kufika sehemu fulani katika maisha yako, nikuambie kwamba hayo mabadiliko uliyopanga hayaji tu kwa kuongea na kuandika kwenye makaratasi bali inahitajika vitendo pasipo vitendo na kung'ang'ana na kile ulichopanga utabakia tu hapo ulipo. Nisikuchoshe na maneno mengi sana, Nikukaribisha ujifunze nami mada ya leo.

Mara nyingi tumepanga kufanya vitu vingi katika maisha yetu, wengine tunapanga kufanya kwa sababu umemwona fulani anafanya sasa na wewe unaamua kufanya na mwingine anapanga kufanya sababu amepanga afanye na anajua akifanya hicho kitu kitamsogeza hatua moja kwenda hatua nyingine katika maisha yake, haya yote ni mambo mazuri maana wengi wetu tunakumbushwa kwa njia ya kuona wenzetu wakiwa wanafanya ama wakiwa wanasema kile wanafanya nasi tunajikuta tunahamasika kufanya kama wao wanavyofanya, hii hutumika kwa watu wengi hasahasa wale wenye kiu ya kubadilika na kuwa tofauti na walivyokuwa jana na wachache sana hupanga vitu vyao na kuanza kuvifanyia kazi pasipo kuangalia nani anafanya na nani havifanyi, wao huamini na husimamia mawazo yao na mipango yao kuhakikisha wanafikia kile walichopanga kufanya katika maisha yao, mara nyingi hawa watu hufika pale walipotarajia na wachache hukwama njiani kwa kukata tamaa pale wanapoona hakuna matokeo mazuri kwa kile walichokianzisha.

Mpaka hapo utakuwa umejijua upo kundi gani kati ya hayo niliyoyasema hapo juu, mimi naomba niongelee wale wengi wetu tunaofanya vitu vingi kwa kuiga kutokana na jamii inayotuzunguka, kwa sababu nia yangu ni kukusaidia/kukufikirisha ujue hicho unachofanya unaelewa unafanya nini au unafanya kwa sababu fulani kafanya au unafanya sababu umepanga kufanya? ni vitu vya msingi kujua sana ili unqpoendelea na safari yako ya kuelekea mafanikio makubwa kwenye eneo ulipo yahitaji kujua kile unafanya, hata kama hutaelewa vizuri kwanini unafanya hicho kitu lazima ujue kile kitu cha mwanzo kilichokusuma kufanya hicho kitu kilikuwa kina maana, ule uamzi wa kwanza uliokupelekea kufanya hicho kitu kizuri chenye manufaa kwako na jamii yako inayokuzunguka ulikuwa uamzi mzuri sana na ndio hicho kitu tunachokiongelea hapa. Mara nyingi kuna vitu tunajikuta tumekolea pasipo kukumbuka ilikuwaje mpaka ukaanza kufanya, jua kuna siku ulitamani kufanya hicho kitu kwa sababu moja ama nyingine iliyokupelekea ukafanya hivyo unavyofanya.

Wewe ambaye umejikuta upo eneo ambalo hujui ufanye nini cha kukuletea maendeleo/mafanikio usiogope sana mimi nipo hapa kukusaidia ujue unafanya nini na ujue utaanzaje kufanya hicho unachotamani kufanya, unapojikuta katika hali hii kaa chini ujiulize unapenda nini? kama hutopata jibu usijali pia na ukipata jibu lakini huoni utaanzia wapi usiogope pia unachotakiwa kufanya kuondokana na hali hiyo ya utata ni kutafuta watu wenye kiu ya mafanikio na wanaomaanisha kwa kile wanafanya, usiogope kujiingiza kwao, usifikiri waliofanikiwa wanatabia ya uchoyo ondoa hayo mawazo kabisa maana asilimia kubwa kwa wana mafanikio wengi huwa wanapenda kusaidia wengine wakue kama wao, furaha yao ni kuona wengine wanaondokana na giza/umaskini wa mawazo waliyonayo maana wanaamini unao uwezo mkubwa ndani yako wa kuleta mabadiliko ya dunia, ndio maana unaona kuna dvd/audio/vitabu vya waliofanikiwa wakieleza kile kimewasaidia kufika hapo walipo na kuna makala kama hizi zikieleza namna ya kutoka hapo ulipo.

Bado unafikiri kuwa hapo ulipo huwezi kutoka? bado huelewi uanzie wapi? Bado utafanya vitu kwa sababu wengi wanafanya? uchanguzi ni wako sasa wa kuamua uwe hivyo ulivyo au kusogea hatua moja kwenda hatua nyingine... maisha haya hayatajua kuwa wewe ulifanya hivyo kwa sababu hukujua basi yatakuhurumia tu upate mafanikio yaani iko hivi kuvunja sheria kwa sababu hukujua kama sheria inasema usitume picha chafu za ngono haikufanyi usichukuliwe hatua za kinidhamu uwe unajua au uwe hujui adhabu ipo palepale kwa hiyo huna budi kujifunza kwa waliofanikiwa, acha kukaa muda mwingi na wenye mawazo mgando, ikiwezekana achana nao kabisa si semi uwachukue bali unahitaji kujitengenezea tabia mpya kwa sasa ukishakomaa vizuri utakuwa na uwezo wa kujua namna yq kuishi nao na utakuwa unajua huwezi kuwaunga mkono vitu gani na utawaunga mkono vitu gani wakati huo watakuwa wanakuona upo hatua nyingine ya kimabadiliko, na itakuwa njia rahisi kuwashuhudia maisha yako ulivyokuwa mwanzo na sasa ulivyo.

Nikutakie mwanzo mwema wa mwezi huu, nikuase kwamba kuwa makini na utumiaji wako wa mitandao kama ulikuwa unatumia mitandao kwa mihemko ya kimwili na hisia mbaya achana na hiyo tabia, itakupeleka pa baya na itakupotezea dira yako ya kufikia malengo yako pale utakapochukuliwa hatua za kisheria.

Waweza wasiliana nami kwa kupiga simu au kunisms kwa njia ya  whatsApp 0759808081 au waweza niandikia email; samsonaron0@gmail.com pia waweza ungana nami facebook Samson Ernest.

Asante na endelea kutembelea mtandao huu wa MTAZAMO WA MAISHA.

SHARE

Samson Ernest

Habari, mimi ni mwandishi na mhamasishaji ambaye ninapenda kuona maisha ya kila mtu yakiwa bora. Naamini kila mmoja wetu anaweza kuwa na maisha mazuri kama ataamua hivyo. Karibu ujifunze kupitia mtandao huu wa MTAZAMO WA MAISHA.

  • Image
  • Image
  • Image
  • Image
  • Image
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

Post a Comment